Tuesday 30 May 2017

Wanaowapa Wanafunzi mimba watangaziwa Kiama Siha




Halmashauri ya Wilaya ya Siha Mkoa wa Kilimanjaro leo tarehe 30 mei,2017 imefanya maazimisho ya juma la elimu kwa kufanya maonesho mbalimbali ya kielimu na kujumuisha wanafunzi wa shule za msingi na Sekondari Wilayani hapa.

Maazimisho hayo yamefanyika Kiwilaya katika shule ya Msingi Sanya juu ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Siha Mhe. Onesmo Buswelu.

Katika hotuba yake katika maazimisho hayo Mkuu wa Wilaya ya Siha Mhe.Onesmo Buswelu alisema kuwa wale wote wanaosababisha mimba kwa wanafunzi sasa wakati umefika wachukuliwe hatua kali za kisheria.

Mkuu wa Wilaya aliongeza kuwa wapo  baadhi ya wazazi kwa kushirikiana na walimu wamekuwa wakiwaficha wahalifu hao mara baada ya kutenda makosa yao.

Aliongeza kuwa kuanzia sasa mtu yeyote atakayesababisha mimba kwa mwanafunzi wa shule Serikali ya Wilaya ya Siha itamsaka popote atakapokwenda na kuhakikisha mtu huyo anachukuliwa hatua za kisheria.

Mhe Onesmo Buswelu Mkuu wa Wilaya ya Siha ametoa wiki mbili kwa wakuu wote wa shule za Sekondari Wilaya ya Siha kumpelekea taarifa za miaka mitatu iliyopita kuhusu hali ya mimba katika shule.

Aliongeza kuwa iwapo atabaini kuwa tatizo la mimba limekuwa likijirudia katika shule moja kwa miaka miwili au mitatu mfululizo basi hata sita kumchukulia hatua stahiki mkuu wa shule husika.

Mkuu wa Wilaya ambaye pia alikuwa mgeni rasmi wa siku ya Elimu Siha alitoa wito kwa  Wazazi kushirikiana na Walimu ili kuboresha kiwango cha ufaulu cha wanafunzi katika shule za msingi na Sekondari Wilayani Siha. Wilaya ya Siha inajumla ya shule 59 za Msingi na  shule 19 za Sekondari.

No comments:

Post a Comment