Wednesday 24 May 2017

Taarifa ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Siha katika Baraza la Madiwani Kipindi cha Januari hadi Machi 2017



OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

HALMASHAURI YA WILAYA YA SIHA



TAARIFA YA MWENYEKITI  WA HALMASHAURI   MKUTANO  WA KAWAIDA WA  BARAZA LA MADIWANI  KATIKA KIPINDI CHA ROBO YA TATU (JANUARI -MACHI,2017).
v  Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Siha,
v  Mwakilishi Ofisi ya RAS-Mkoa wa Kilimanjaro,
v  Mh. Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Siha,
v  Mh. Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Siha,
v  Waheshimiwa Madiwani,
v  Mkurugenzi Halmashauri ya Siha,
v  Viongozi wa Dini,
v  Wageni Waalikwa,
v  Ndugu Wataalamu,
v  Waandishi wa Habari,
v  Wananchi wa Wilaya ya Siha,
v  Mabibi na Mabwana,

Wasalaam Alekumu,Tumsifu Yesu Kristo,Bwana Yesu asifiwe

Wah. Madiwani ,  na Ndugu  Wananchi;
Kwanza kabisa napenda kuwakaribisha Waheshimiwa Madiwani,Wananchi,Wadau wa maendeleo,Wataalam wa Halmashauri na Waandishi wa Habari katika  Mkutano  wa Kawaida wa Baraza la Madiwani katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2016/2017 (Januari hadi Machi,2017). Katika kipindi hiki tumeshuhudia Halmashauri yetu ikiendelea na shughuli zake za kuwapatia Wananchi wa Wilaya ya Siha huduma mbalimbali zikiwemo za Afya,Elimu,Maji na huduma nyinginezo. Kipekee napenda kuwapongeza Waheshimiwa Madiwani na Wataalam wa Halmashauri ya Siha kwa kuiwezesha Halmashauri ya Siha kupata hati Safi na kuwa miongoni mwa Halmashauri za Mkoa wa Kilimanjaro na Tanzania. Naomba kwa pamoja tuendelee kushirikiana  Viongozi na Watumishi ili kuhakikisha kuwa Halmashauri yetu inaendelea kufanya vizuri na kupata hati safi kwa miaka mingi ijayo.  

(1)UKUSANYAJI WA MAPATO
Waheshimiwa Madiwani,
Kama mnavyojua Waheshimiwa Madiwani na ndugu  Wananchi wa Siha kuwa bado Halmashauri yetu inakabiliwa na kuwa na tatizo la kuwa na vyanzo vichache na vya kudumu kwa ajili kukusanya Mapato ya ndani ya Halmashauri. Nawaomba tena kwa umoja wetu tuendelee kubuni vyanzo mbalimbali vya kuongeza mapato ya ndani ya  Halmashauri  yetu ili itusaidie kuboresha huduma mbalimbali kwa Wananchi wetu. Ukweli ni kwamba vyanzo  vya mapato ya ndani vilivyopo sasa  kama vile ushuru wa Masoko,Ushuru wa mazao,Leseni na Vituo vya Mabasi siyo vyanzo vya kutegemewa sana kwani mapato tunayopata kutoka vyanzo hivi bado ni kidogo sana. Napenda kutoa Rai kwa viongozi wenzangu tufikirie zaidi nakuwa wabunifu zaidi hasa namna ya  kupata fedha kutoka kwa Mashamba makubwa yaliyopo Wilayani Siha na tufanye juhudi kuhakikisha masuala ya uwekezaji katika Wilaya yetu yanaimarika zaidi hasa ule mradi mkubwa wa kituo cha Utalii. Tusipofanya juhudi za makusudi kwenye suala la kuongezaukusanyaji wa Mapato ya ndani ya Halmashauri naona uwezekano mkubwa wa Halmashauri yetu kushindwa kutoa huduma zinastahili za kuwaletea Wananchi maendelea hasa katika Kata na Vijiji vyetu.

 (2) UTUNZAJI WA MAZINGIRA
Waheshimiwa Madiwani,ndg  Wananchi na Wataalam.
Napenda kuendeleza kuwahimiza Wananchi na Wakazi wote wa Wilaya ya Siha kutumia vizuri baraza za Mvua zinazoendelea kunyesha hivi sasa katika Wilaya yetu kwa  kupanda miti ya kutosha ili kuimarisha mazingira yetu na kurudisha uoto wa asili kama ilivyokuwa hapo miaka ya nyuma. naomba kurudia tena ombi langu kwa Wananchi na Wakazi wa Wilaya ya Siha kuhakikisha  kila kaya kuotesha angalau miti 5 kila mwaka na kama inawezekana tuweke kwenye sheria ndogo za Halmashauri ambazo zitamtaka kila mwenye eneo la ardhi kuotesha miti ya kutosha kulingana na ukubwa wa eneo lake. Kwa hili naomba kurudia kwa kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Siha kuhakikisha kuwa Watendaji wa Kata na Vijiji katika Halmashauri ya Siha  kupitia vikao vya Vijiji na Vitongoji wanawaelimisha wananchi kuhusu upandaji wa miti katika maeneo yao. Ndugu Mkurugenzi agizo langu hili nitalifuatilia kwa karibu kuona jinsi gani Serikali za Vijiji na Kata limelitekeleza kwa Vitendo na wale wote watakaoshindwa kutekeleza naomba wachukuliwa hatua stahiki kwani wanapinga suala zima la kuboresha mazingira ya Wilaya yetu. Nawaomba Viongozi wenzangu tushirikiane kwa pamoja kuwaelimisha Wananchi katika Kata na Vijiji tunapotoka ili kufanikisha zoezi hili muhimu kwa ustawi wa Wilaya yetu ya Siha..
Aidha, najua adui mkubwa wa miti ni mifugo,naomba wote kwa pamoja tusaidiane kulinda mifugo  yetu ili isiharibu miti tunayopanda kila mwaka katika maeneo yetu. 

Waheshimiwa Madiwani,Ndugu Wananchi;
(3)ELIMU
Katika suala la Elimu,Naombakutoa wito kwa wazazi na Walezi kutimiza wajibu wao ili kuhakikisha kuwa watoto wao mashuleni wanapata mahitaji muhimu kama vile,Madaftari,Kalamu,Sare za shule pamoja na chakula cha mchana wakiwa shuleni. Hili nalirudia mara kwa mara kwa kuzingatia umuhimu wa elimu katika maisha ya kila siku ya binadamu,Jamii na Taifa kwa ujumla wake.Sambamba na hilo hivi karibuni kumefanyika Mtihani wa  Taifa wa Kidato cha Sita katika shule zetu za Oshara,Nuru,Sanya Juu na Magadini na taarifa nilizopata ni kuwa mitihani hiyo imefanyika kwa utulivu wa hali ya juu na hakuna jambo lolote lililo nje ya utaratibu limeripotiwa. Kwa hili naipongeza ofisi ya Mkurugenzi kwa kusimamia zoezi hili hadi limefanyika kwa ufanisi Mkubwa,Hata hivyo ni matumaini yetu kuwa matokeo ya Mtihani  huo yatakuwa mazuri katika shule zetu za Wilaya ya Siha pindi yatakapotangazwa na Idara/Wizara husika. Vilevile nimepata taarifa kuwa Mitihani ya Majaribio ya Mkoa kwa Wanafunzi wa Kidato cha nne (Mock) inatarajiwa kuanza hivi karibuni katika shule zetu za Sekondari Wilaya ya Siha. Naomba kuwatakia Wanafunzi wote wa Kidato cha Nne kwa mwaka huu kujiandaa vema kwa mitahani hiyo na Hatimaye kupata matokeo mazuri yatakayoiwezesha Wilaya ya Siha kupata ufaulu mzuri. ’’ Elimu ni ufunguo wa maisha kila  mtu atimize wajibu wake ’’.

(4) UTUNZAJI WA BARABARA
Waheshimiwa Madiwani,Ndugu Wananchi;
 Naomba tena kuwakumbusha wananchi wa  Halmashauri ya Siha kuhakikisha kuwa kila mmoja anashiriki kikamilifu katika  kuzitunza barabara zilizojengwa na Serikali katika Kata na Vijiji vyetu. Pamoja na kuwa na Changamoto ya mvua zinazoendelea kunyesha katika Wilaya yetu bado tunao wajibu wa kuendeleza kuzitunza barabara zilizopo katika maeneo yetu. Kwa mfano utakuta mfereji wa maji umepasuka na maji yanaelekea barabarani lakini mara nyingine kwa mshangao Serikali za maeneo husika hazichukui hatua zinazotakiwa za kuziba maji hayo. Naomba kutoa Wito kwa Watendaji wa Vijiji na Kata kwa kushirikiana na Wananchi wahakikishe kuwa barabara zote zilizopita maeneo ya Vijiji na Kata zao zinalindwa hata kwa kuwapa adhabu wale wote wanaoharibu barabara kwa makusudi.   
Naomba kutoa agizo kuwa kuanzia sasa ni marufuku kwa mtu yeyote  kukata barabara bila kibali cha Mkurugenzi Mtendaji  na yeyote atakayekiuka agizo hili basi  achukuliwe hatua ili iwe fundisho kwa wenzake. Mkutano wa baraza lililopita liliagiza tena hili lakini sijapata taarifa ya Waharibifu wangapi wa barabara wamechukuliwa hatua za kisheria.

(5)UWAJIBIKAJI KAZINI
Waheshimiwa Madiwani,Ndugu Wananchi;
Kama ilivyokuwa katika taarifa zangu kwa Baraza la Madiwani,napenda kuwakumbusha tena Watumishi wa Serikali waliopo Wilaya ya Siha kuwa Serikali ya awamu ya tano imeshasema kuwa haitawavumilia Watumishi wazembe na wabadhirifu kazini. Naomba kila mtumishi atimize wajibu wake kwa mujibu wa taaluma aliyosomea na kwa kufuata sheria na taratibu za utumishi wa Umma. 

Aidha ,naomba kumwagiza Mkurugenzi kuwa Watumishi wote waliobainika kuwa na vyeti visivyo sahihi(vyeti Feki) wasiruhusiwa kuwepo maeneo ya kazi katika halmashauri yetu kama agizo la Mhe. Dkt John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alilolitoa siku ya Mei Mosi katika uwanja wa Chuo cha Ushirika Mjini Moshi. Mheshimiwa Rais aliagiza kuwa watumishi hao wasionekane maeneo ya kazi ifikapo Mei 15,2017 na atakayeonekana atachukuliwa hatua za kisheria. Mkurugenzi hili ni lako nakuomba usimamie kwa karibu kama bado unaipenda kazi yako ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji,mimi kama Mwenyekiti wa Halmashauri ya Siha nimeona nikukumbushe hilo ili ufuatilie kwa karibu zaidi.

Waheshimiwa  Madiwani na ndg Wananchi;
Kabla ya kufika mwisho wa Taarifa yangu, napenda  kuwashukuru tena Wananchi wa Wilaya ya  Siha na Waheshimiwa Madiwani  kwa ushirikiano  wenu wa dhati mnaoendelea kunipatia kwa ajili ya kutekeleza majukumu yangu ya Kila siku. Naomba kuchukua fursa hii kuwahimiza Wananchi wa Siha  kuzitumia vema mvua zinazonyesha kwa ajili ya mazao ya chakula na biashara bila kusahau uoteshaji wa miti katika maeneo yetu ili kulinda mazingira. Kwani ipo kauli ya mazingira inayosema ’’MISITU NI UHAI’’. Naomba wote kwa umoja wetu tufanye kazi kwa kushirikiana ili kuharakisha maendeleo yetu pamoja na maendeleo ya  Familia zetu , Wilaya ya Siha na Taifa kwa ujumla wake.
Mwisho kabisa  ,nichukue fursa hii kwa niaba ya baraza la Madiwani, kuwashukuru tena kwa usikivu wenu mkubwa mlionesha tangu mwanzo wa taarifa yangu, naomba usikivu na utulivu huu uendelee hadi mwisho wa Mkutano wetu na hatimaye tumalize na kuagana kwa upendo na furaha.
Asanteni sana kwa kunisikiliza
Imetolewa na:
Frank K. Tarimo
Mwenyekiti wa Halmashauri (W)
SIHA

No comments:

Post a Comment