Tuesday 16 May 2017

Wananchi kukamilisha Ujenzi wa Maabara



Wananchi wa Kata ya Kirua Wilayani Siha pamoja na Wazazi wa wanafunzi wanaosoma katika shule ya Sekondari Fuka wamekubaliana kwa kauli moja kukamilisha kazi ya ujenzi wa maabara tatu za masomo ya Sayansi katika shule hiyo.

Kauli hiyo imetolewa na Wananchi hao walipokuwa Wakiongea katika Mkutano wa Mkuu wa Wilaya ya Siha alioufanya katika shule ya Sekondari Fuka tarehe 16.5.2017.

Awali Mkuu wa Shule hiyo  mwalimu Swalehe Kombo  alisoma taarifa fupi ya maendeleo ya ujenzi wa Maabara katika shule hiyo ambapo alieleza kuwa zaidi ya shilingi milioni 5 zimetumika katika kuendeleza ujenzi wa maabara katika kipindi cha Novemba,2016 hadi Mei 15,2017.

Mkuu wa Shule hiyo alimweleza Mkuu wa Wilaya kuwa,  Wananchi wa Kata ya Kirua wameweka mpango wa kupata michango ya Shilingi elfu tano kwa kila kaya ,ambapo kupatikana kwa fedha hizo kutasaidia kuendeleza ujenzi wa Maabara katika shule hiyo.

Akiongea na Wananchi na Wazazi wa wanafunzi wanaosoma shule ya Sekondari Fuka iliyopo   Kata ya Kirua,Mkuu wa Wilaya ya Siha Mhe. Onesmo Buswelu aliwapongeza Wananchi kwa kuwa kuonyesha hali ya kujituma na moyo  ya kuchangia maendeleo hasa katika suala la elimu kwa watoto wao.

Mkuu huyo wa Wilaya alieleza kuwa Serikali itaendelea na jitihada zake za kushirikiana na Wananchi pamoja na wadau wa maendeleo katika kuleta maendeleo, na katika ujenzi wa maabara Serikali imeahidi kuleta vifaa vyote katika maabara hizo.  Alifafanua kuwa vifaa vya maabara vitakavyoletwa na Serikali ni vya gharama kubwa na vitahitaji kutunzwa na kuhifadhiwa kwa uangalifu na shule husika zitakazokabidhiwa.

Wilaya ya Siha inajumla ya shule 13 za Serikali ambapo kila shule inahitaji kuwa na maabara 3 kwa masomo ya Biolojia,Chemia na Fizikia kama ilivyo agizo la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

No comments:

Post a Comment