Thursday 25 May 2017

Taarifa kwa Umma kuhusu Kazi zilizotekelezwa na Serikali Wilayani Siha-Mkoa wa Kilimanjaro



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA RAIS TAMISEMI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KAZI ZILIZOTEKELEZWA NA SERIKALI WILAYANI SIHA

Ndugu Wanahabari,na Wananchi
Napenda kuchukua fursa hii  kuwakaribisha sana katika Wilaya ya Siha  ili niweze kukutana nanyi kwa lengo la kutoa taarifa  ya mambo mbalimbali ya maendeleo yanayoendelea katika Wilaya ya Siha tangu Serikali ya Awamu ya tano ilipoingia madarakani chini ya Mhe. Dkt John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kabla sijaanza kutoa taarifa yangu naomba kuishukuru Serikali yetu kwa kutupatia fedha  za kutekeleza miradi ya maendeleo katika Wilaya yetu ya Siha.

Pili napenda kuwashukuru Wananchi wote wa Wilaya ya Siha kwa kushirikiana na Serikali yao katika shughuli za miradi ya  maendeleo pamoja  na suala zima la utunzaji wa Amani katika Wilaya yetu.

Ndugu Wanahabari
Nianze na hali ya ulinzi na usalama, kwa ujumla Wilaya ya Siha ni salama kabisa na hakuna tukio lolote ambalo limetokea la kuhatarisha amani na hii imetokana na tabia njema ya Wananchi wa  Wilaya ya Siha kama walivyo Watanzania wengine kuwa na utamaduni wa kudumisha amani, kipekee nawashukuru Wananchi na wakazi wa Wilaya ya  Siha kwa kuendelea kudumisha amani wakati wote hasa katika sikukuu ya Pasaka  mwaka huu 2017 iliyofanyika tarehe 16-17/04/2017, ambapo kuwepo kwa amani kumesaidia  Wananchi   kuendelea na shughuli za kiuchumi ambazo zinawapatia kipato ikiwemo shughuli za  Kilimo,Ufugaji  na biashara ndogondogo.
Ndugu Wanahabari,
Katika kutekeleza miradi ya maendeleo Serikali ya awamu ya tano imewezesha miradi mbalimbali kukamilika na mingine inaendelea kukamilishwa katika hatua mbalimbali. Miongoni mwa miradi iliyotekelezwa na serikali ya awamu ya Tano Chini ya Mhe.Dkt John Pombe Magufuli ni kama ifuatavyo;-

1.   Katika sekta ya Kilimo,Ushirika na Umwagiliaji,Serikali imewezesha na kuleta fedha Wilayani Siha  kiasi cha Tshs. 165,000,000/= zilizowezesha kukamilisha ujenzi wa mita 1000 za mfereji wa maji ya Umwagiliaji Kijiji cha Kishisha Kata ya Ivaeny.  Pia Serikali imetoa fedha kiasi cha Tshs 165,000,000/= kwa ajili ya ujenzi wa  mfereji wa umwagiliaji Kijiji cha Mowonjamu Kata ya Livishi  wenye urefu wa mita 700 na kujenga bwawa la kuhifadhia maji . Baadhi ya Kazi zimekamilika na nyingine zipo katika hatua mbalimbali za ukamilishaji.  Vile vile kama mnavyoona mvua kwa sasa ni nyingi na mazao mashambani yanaendelea vizuri na matajio yetu kama Wilaya ya Siha  ni kupat tani 102,705 kwa mazao ya chakula na Biashara, Pia Wilaya inategemea kupata tani 10,126 kwa mazao ya Bustani na mbogamboga. Pia kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha kwa wingi katika Wilaya yetu ya Siha naomba kutoa wito kwa Wananchi kuchukua tahadhari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza hasa kuangalia Wanafunzi wanaokwenda shuleni asubuhi wasije kuzolewa na maji.
2.   Mfuko wa Wanawake na Vijana. Katika kipindi kifupi tangu Serikali ya awamu ya Tano kuingia madarakani Jumla ya FedhaTsh. 75,000,000/= zimetolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Siha Siha kwa ajili ya Kusaidia vikundi mbalimbali vya Wanawake na Vijana. Katika Fedha hizo jumla ya vikundi 20 vya Wanawake vyenye wanufaika 316 wamepatiwa mikopo, Pamoja na vikundi 7 vya vijana vyenye wanufaika 130 vimewezeshwa kupitia asilimia 10 ya Mapato ya Ndani ya Halmashauri ya Siha. Hata hivyo Nimetoa agizo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Siha kuhakikisha kuwa asilimia 5 ya vijana na 5 ya Wanawake inatolewa katika Makusanyo ya Mapato ya ndani ya Halmashauri ili kuwezesha  kuongeza wanufaika wengi zaidi katika Makundi ya Vijana na Wanawake.

3.   Katika Sekta ya Afya; Tunaishukuru Serikali kwa kutupatia fedha jumla ya Tsh. 250,000,000/= kwa ajili ya kukamilisha jengo la OPD sakafu ya juu katika Hospital yetu ya Wilaya ya Siha. Kazi hii inafanyika kwa kupitia “force account” na inasimamiwa na Wataalam  na Watumishi wa Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Siha. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwezi Juni,2017. Serikali ya Wilaya ya Siha imeamua kutumia “force account” ili kuhakikisha kuwa fedha za Serikali zinatumika vizuri na kutoa thamani halisi ya fedha. Aidha kwa upande mwingine Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Siha kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji imepanga kufanya harambee ambayo itawezezesha ujenzi wa majengo matatu (Wodi ya Wazazi,Wodi ya Watoto na Jengo la upasuaji) Majengo haya yana thamani ya Fedha za Kitanzania 880,000,000/=. Mpango huu umeshirikisha  Wanannchi wa Wilaya ya Siha, wadau wa maendeleo wa ndani na nje ya Halmashauri pamoja na Watumishi wa Wilaya ya Siha. Lengo la mpango huu ni kuwaondolea usumbufu na kuwapunguzia  Wananchi wa Siha gharama za matibabu kwa wagonjwa wao hasa wanapopewa rufaa  katika Hospital ya Mkoa Mawenzi na Hospital ya Rufaa ya KCMC mjini Moshi.
Hata hivyo hadi sasa Jumla ya Tsh. 52,000,000/= zimepatikana  na vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya Tsh 11,000,000/= vimetolewa na wadau mbalimbali na Wananchi ,huku ahadi zenye thamani ya Tsh milioni 62 zikitarajiwa kupokewa ili kukamilisha ujenzi huo. Hata hivyo michango iliyotolewa, ahadi na vifaa vilivyotolewa zinafikia jumla ya Tshs 125,000,000/=.Hadi sasa ujenzi wa wodi ya wazazi  umeanza na ujenzi wa  Msingi umekamilika na kazi ya ujenzi inategemewa kukamilika mwezi Julai,2017 kama wadau na wananchi waliotoa ahadi zao watakamilisha kwa wakati. Hata hivyo Serikali imeongeza kiwango cha ununuzi wa dawa katika Zahanati na vituo vya Afya vya Serikali kutoka asilimia 25% mwaka 2016 hadi kufikia asilimia 85% mwaka huu.

Ndg Wanahabari. Napenda kuwashukuru Wananchi wa Siha kwa ushirikiano wa dhati walionesha katika ujenzi wa  kazi hii muhimu, na napenda kutoa wito kwa Wananchi,Watumishi na Wadau wengine wa maendeleo kukamilisha ahadi zao walizotoa ili kufanikisha mpango huu wa ujenzi kwa wakati. Vilevile natoa wito kwa Wananchi na wadau wengine nje na ndani ya Wilaya kutuunga mkono katika ujenzi wa Hospital ya Wilaya ya Siha. 

4.   Sekta ya Elimu. Serikali ya awamu ya Tano imeendelea kutimiza azma yake ya kutoa elimu bure kuanzia darasa la awali hadi kidato cha Nne kwa kuhakikisha kuwa Mahitaji muhimu ya shule yanapatikana  kama vile vitabu,mishahara ya Watumishi,vifaa muhimu vya maabara mpya zilizojengwa, mafunzo kwa watumishi hasa Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari yametolewa ili kuwajengea uwezo. Katika sekta ya Elimu, Serikali ya awamu ya tano imeweza kujenga nyumba mbili za Walimu(Six in one) katika shule za Sekondari Suumu na Namwai kwa gharama ya Tsh.300,000,000/=, hadi sasa nyumba hizo zimekamilika na  zimeanza kutumika na Walimu wa shule husika. Pia Serikali imetoa fedha  jumla ya Tsh. 24,000,000/= za ukarabati wa  madarasa matatu katika shule ya Sekondari Suumu na kazi imekamilika. Vile vile Serikali imetoa Tsh. Milioni 36 kwa ajili ya ujenzi wa matundu 18 ya vyoo katika shule ya Sekondari Namwai na Suumu(Namwai matundu 16 na Suumu matundu 2). Kwa kipindi hiki pia Serikali imetoa Jumla ya Tsh milioni 71 za ujenzi wa Bweni la Wanafunzi katika shule ya Sekondari Oshara, kazi hii inaendelea na inatarajiwa kukamilika mwezi Julai 2017. Katika kuboresha Elimu  Serikali imetoa jumla  ya madawati 537 Wilayani Siha ili kuonesha kwa vitendo azma ya kuboresha elimu kwa jamii ya watanzania. Madawati haya yamegawanywa katika shule za Msingi na Sekondari za Serikali Wilaya ya Siha na kusaidia kuondoa upungufu wa  madawati uliokuwepo hapo awali. Hadi sasa Wilaya ya Siha inayo madawati ya ziada 747 kwa kujumuisha Elimu Msingi na Sekondari. Halmashauri ya Wilaya ya Siha inapokea kila mwezi jumla ya Kiasi cha Fedha za Kitanzania shilingi  38,093,000/= Katika kutekeleza elimu bila malipo katika shule za Sekondari na Kiasi cha Shilingi 29,187,000/= hutolewa na Serikali Kila mwezi ili kugharamia   elimu kwa shule za msingi. Pia Serikali imetoa jumla ya vitabu 6834 kwa shule za  Sekondari Wilaya ya Siha katika masomo ya Sanaa na Sanyansi. Wito wangu kwa Wanafunzi wote waliopo mashuleni kuhakikisha kuwa wanasoma kwa bidii na maarifa kwani jamii na Taifa linawategemea wao katika kuleta maendeleo ya familia zao,Jamii na Taifa kwa Ujumla wake. Pia nawahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii ili kuondokana na kuwa na vyeti Feki kama baadhi ya watumishi wa Umma walivyogundulika katika maeneo mbalimbali hapa Nchini kuwa na vyeti feki, hii ilitokana na wao kutosoma kwa bidii wakati wakiwa wanafunzi. 

Ndugu Wanahabari;
Vilevile katika kuboresha miundombinu ya barabara Serikali ya Awamu ya tano chini ya uongozi bora wa Mhe John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeanza ujenzi wa barabara ya kiwango cha  Lami kutoka Sanya Juu hadi Elerai yenye urefu wa Km 32.2 kwa gharama  ya fedha za Kitanzania shilingi bilioni 52.3. Ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha Lami umeanza rasmi mwezi Machi mwaka huu na unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba,2018. Kukamilika kwa barabara hii kutasaidia kufungua fursa za uchumi katika Tarafa ya Siha Magharibi na Wilaya ya Siha kwa ujumla, hasa kusaidia kupitisha watalii zaidi wanaopanda mlima Kilimanjaro kupitia lango la Londorosi pamoja na kurahisisha kusafirisha mazao mbalimbali yanalimwa kwa wingi katika mashamba makubwa ya West Kilimanjaro. Pia Serikali imeendelea kutoa fedha za kuwezesha  ujenzi wa barabara ndani ya wilaya ya Siha  kwa viwango vya Changarawe, miongoni mwa barabara hizo ni kama ifuatavyo;-i)Ujenzi wa barabara ya Kifufu Mowonjam na Ngirini, Nsherehehe hadi Ngarony yenye urefu wa km 14.6 kwa gharama ya fedha za Kitanzania shilingi 829,954,000/= na  kazi ya ujenzi imekamilika. (ii)Barabara ya Karansi Tanki la maji yenye urefu wa  Km 6.4 iliyogharimu kiasi cha Tshs.  633,024,100/=imekamilika (iii) Pia  Serikali  imetoa fedha zilizowezesha ujenzi wa Kalvati kubwa la Kisube Kirisha na ujenzi wa  barabara yenye urefu wa  Km 2.5 kwa gharama ya shilingi za Kitanzania 920,172,587.50/= kazi hii ya ujenzi imekamilika na ipo katika kipindi cha uangalizi.

Ndugu Wanahabari:
Aidha, katika miradi ya Maji Serikali ya awamu ya tano imetoa fedha Kiasi cha Tsh. 1,682,062,000/= Wilayani Siha kwa ajili ukarabati na upanuzi wa mradi wa maji Magadini Makiwaru katika vijiji vya (Wiri,Mawasiliano,Lekrimuni,kandashi na Orkolili) na mradi wa Maji lawate Fuka katika vijiji vya Kishisha,Donyomuruak,Embukoi,Ngaritati na Naibili). Kazi za ukarabati katika miradi hii ya maji imekamilika na Wananchi wa Siha wanapata maji safi na Salama katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Siha.
Ndugu Wanahabari,
Katika mpango wa Serikali wa kunusuru Kaya Maskini kupitia Mradi wa TASAF III,Jumla ya Kaya Maskini 1871 Wilaya ya Siha zimewezeshwa na kunufaika na mpango huu wa Serikali wa kunusuru Kaya Maskini na Jumla ya Fedha za Kitanzania Shilingi 691,638,636/= zimetumika. Kwa niaba ya Wananchi wa Wilaya ya Siha napenda kutoa shukrani za dhati kwa Serikali yetu tukufu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kusaidia jamii ya Watanzania hasa kaya zisizo na uwezo. Wito wangu kwa wanufaika wa mpango huu, napenda kuwaasa wanufaika wote kuwa na nidhamu bora ya matumizi ya fedha wanazopatiwa na Serikali kupitia mpango huu. 

Ndugu Wanahabari:
Soko la Sanya Juu, katika kuboresha miundombinu ya soko kuu la Wilaya ya Siha yaani    soko la Sanya Juu,Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayosimamiwa na Chama Cha Mapinduzi  imetoa jumla ya shilingi 71,161,200/= kwa Halmashauri ya siha ili kusaidia kuboresha miundombinu katika soko hilo. Kwa sasa taratibu zinaendelea na kazi hiyo inatarajiwa kuanza mwezi wa Juni,2017. Mimi Mkuu wa Wilaya ya Siha na msimamizi wa shughuli za Serikali Wilaya ya Siha nimemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kazi hiyo inafanyika kwa viwango vinavyotakiwa ili kuonyesha thamani halisi ya fedha za Umma zilizotolewa.

Ndugu Wanahabari:
Katika hatua za kuharakisha maendeleo ya Wananchi Wilaya ya Siha,Serikali kwa mwaka huu wa fedha 2016/2017 imetoa  Fedha za mfuko wa Jimbo jumla shilingi 29,084,000/= kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo ya Wananchi katika Kata na vijiji mbalimbali Wilayani Siha. Kwa niaba ya Wananchi wa Siha napenda tena  kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuletea fedha za mfuko wa Jimbo ambazo kimsingi zinatusaidia sana katika maendeleo ya Wananchi ya Wilaya yetu ya Siha.
Ndugu Wanahabari:
Serikali ya Wilaya ya Siha inapenda kuwashukuru Wananchi na Wakazi wa wote wa Wilaya Siha, wadau wa maendeleo pamoja na Sekta Binafsi  kwa kutoa ushirikiano hasa katika shughuli za maendeleo bila kujali tofauti za itikadi za Kisiasa ,maeneo watu wanapotoka na imani zetu za madhehebu ya Dini. Kwa kufuata misingi ambayo baba wa Taifa mwalimu Julius K Nyerere alituachia, Wilaya ya Siha tunategemea kuendelea  kupata maendeleo makubwa ndani ya muda mfupi ujao. Naomba kutoa wito kwa Wananchi, Wadau wa maendeleo  na Viongozi wote Wilayani Siha kudumisha mshikamano uliopo ili kutimiza malengo ya Serikali ya awamu ya tano katika kuwaletea Wananchi wake maendeleo ya kweli. 

Ndugu Wanahabari:
Vilevile, kabla ya kufikia mwisho wa taarifa yangu,naomba kutoa wito kwa Watumishi wote wa Umma kufanya kazi za kuwahudumia Wananchi  kwa uadilifu na weledi mkubwa ili kulinda heshima ya Watumishi wa Umma na Serikali kwa ujumla.  Serikali ya awamu ya tano haipo tayari kuwavumilia watumishi wazembe,wavivu ,walarushwa pamoja na wale wote wanaofanya kazi kwa mazoea.

Ndugu Wanahabari,
Mwisho Serikali ya Wilaya ya Siha kwa kuzingatia muongozo wa Ilani ya Chama  cha Mapinduzi (2015-2020) itaendelea kusimamia na kuratibu miradi yote ya maendeleo ili kuhakikisha kuwa fedha za Serikali zinatumika kwa malengo tu yaliyokusudiwa. Natoa wito kwa watumishi wote wa Umma Wilayani Siha kuhakikisha kuwa wanasimamia Ilani ya Chama Tawala na kutimiza malengo yaliyowekwa na Serikali ya awamu ya Tano chini ya uongozi bora wa Mheshimiwa John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mungu ibariki  Afrika,Mungu ibariki Tanzania na Mungu ibariki Wilaya ya   Siha
asanteni sana kwa kunisikiliza
Imetolewa na:-
Mhe; ONESMO M. BUSWELU
MKUU WA WILAYA YA SIHA
Leo tarehe 12/05/2017

No comments:

Post a Comment