Monday 24 October 2016

WADAU WACHANGIA ELIMU WILAYANI SIHA-KILIMANJARO





Wadau wachangia elimu shule ya sekondari Magadini

Wadau mbalimbali wa elimu Wilayani Siha wamechangia fedha za ukarabati wa miundombinu ya shule ya Sekondari Magadini iliyopo Kata ya Gararagua Wilayani Siha Mkoa wa Kilimanjaro.

Harambee hiyo iliandaliwa na Bodi ya Shule ya Sekondari Magadini kwa ushirikiano na Uongozi wa Shule  hiyo pamoja na uongozi wa Kata  na Vijiji. 

Katika harambee hiyo iliyofanyika mwishoni mwa wiki katika Shule ya Sekondari Magadini zaidi ya Tsh. Milioni 5 zilikusanywa, fedha hizi  zinajumuisha fedha taslimu,ahadi na vifaa vya ujenzi vilivyotolewa  na wadau .

Awali akitoa taarifa  fupi kwa mgeni rasmi katika harambee hiyo mkuu wa shule Felista Kileo  alieleza kuwa wameona ni vema kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya tano katika kuboresha miundombinu ya shule hiyo ili kuboresha  mazingira ya kujifunza na kufundishia.

Alieleza kuwa fedha na vifaa mbalimbali vilivyopatikana vitasaidia katika kuboresha na kukarabati madarasa kachakavu katika shule hiyo yenye wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita.

Katika harambee hiyo ,Mkuu wa Wilaya ya Siha Mhe. Onesmo Buswelu alichangia mifuko 35 ya saruji yenye thamani ya shilingi 525,000/= ambapo mchango wake ulikabidhiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya  Siha.

No comments:

Post a Comment