Wednesday 11 May 2016

WATOTO ZAIDI YA 24000 KUPATIWA CHANJO YA MINYOO SIHA

Wilaya ya Siha inategemea kutoa chanjo ya minyoo kwa watoto zaidi ya 24000 kwa mwaka 2016.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Siha Rashid Kitambulio  amewataka wananchi na wakazi wote wa Siha kutoa ushirikiano wa kutosha ili kufanikisha zoezi hilo muhimu kwa maendeleo ya watoto wetu na Taifa kwa ujumla.

Mkurugenzi amewataka wazazi kuhakikisha kuwa watoto wote wenye umri wa miaka 4 hadi 14 wanapatiwa chanjo hiyo muhimu kwa ajili ya minyoo. alieleza kuwa wataalam wa afya kwa kushirikiana na Walimu watahakikisha wanasimamia zoezi hilo kwa ukamilifu ili kutimiza malengo ya kuwachanya watoto wote katika Wilaya ya Siha.

alitoa wito kwa wazazi kushirikiana na watoa huduma ili kila mtoto anayestahili apatiwe chanjo kwa wakati. Aliongeza kuwa chanjo hiyo inatolewa bure bila malipo yoyote na kuwatoa hofu wazazi wanafikiri kuwa watatakiwa kufanya malipo.

Hata hivyo mkurugenzi wa Halmashauri ya Siha alieleza kuwa matayarisho ya vifaa vyote vinavyotakiwa vimekamilika na zoezi limeanza leo tarehe 11.05.2016 katika kata zote 17 zilizopo Wilayani Siha. Alisema kuwa zoezi hilo litaendelea tarehe 12 na 13 kama halitakamilika kwa siku moja lengo ni kuhakikisha kuwa walengwa wote wanapata huduma.



No comments:

Post a Comment