Wednesday 6 December 2017

Watumishi wa Umma Walevi kuchukuliwa hatua



WATUMISHI WA UMMA WALEVI WAONYWA SIHA

Watumishi wa Serikali wanaotumia pombe muda wa kazi Wilaya ya Siha wamepewa karipio la kuacha tabia hiyo mara moja vingenevyo watachukuliwa hatua za kinidhamu.

Hayo yamesemwa na mkuu wa Wilaya ya Siha  mhe. Onesmo Buswelu katika ukumbi wa Kanisa katoliki  Sanya Juu alipokutana na walimu wa shule za Msingi Wilaya ya Siha siku ya jumatatu tarehe 04 desemba,2017.

Katika kikao kazi hicho kilichokuwa na lengo la kufanya tathmini ya matokeo ya darasa la saba mwaka 2017 pamoja na kutafuta mbinu za kuboresha kiwango cha ufaulu katika shule za msingi.

Mkuu wa Wilaya ya Siha alieleza kuwa wapo watumishi wa umma wakiwemo walimu ambao wanafika kazini wakiwa wamekunywa pombe ,jambo ambalo haliruhusiwi kisheria kwa watumishi wa Umma.

Alitoa wito kwa watumishi wote wa Umma Wilayani Siha wenye tabia ya ulevi kazini kuacha kitendo hicho cha aibu mara moja,kwani wasipofanya ivyo Serikali haitasita kuwachukulia hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kuwasimamisha kazi  na hata  kuwafukuza kazi kabisa.

Mhe Mkuu wa Wilaya  Siha aliwataka walimu wa Wilaya ya Siha kuendelea kuwa mfano bora katika kuzingatia maadili ya kazi ya ualimu pamoja na kuchapa kazi kwa bidii na maarifa huku wakijua kuwa serikali na jamii inawategemea walimu katika kujenga jamii imara na mathubuti.

Vile vile, aliwahakikishia walimu wa Wilaya ya Siha, kuwa Serikali ya awamu ya Tano chini ya Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imedhamiria kuondoa kero mbalimbali za walimu ikiwa ni pamoja na kuwapa walimu  huduma kwa wakati pale wanapohitaji pamoja na kuboresha maslahi ya walimu.

Kwa upande wa jamii,Mkuu wa Wilaya alitoa wito kwa jamii na wazazi kuhakikisha kuwa wanafuatilia maendeleo ya kitaaluma ya  watoto wao mashuleni kwa lengo la kuongeza ufaulu.

Napenda kutoa agizo kwa watendaji wa Vijiji wakishirikiana na Serikali za Vijiji vyote Siha kuwachukulia hatua za kisheria wazazi wote wanaoacha kuwaandikisha shule watoto wenye umri wa kwenda shuleni alisema Buswelu.

Aidha aliwataka walimu kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Tanzania katika uboreshaji wa elimu hasa kwa walimu kufanya kazi kwa kujituma kama ilivyo katika maadili ya kazi hiyo.

No comments:

Post a Comment