Thursday 26 October 2017

Wanawake Wapatiwa Mikopo




Vikundi 22 Wanawake vyapatiwa mikopo  2016/2017

Halmashauri ya Wilaya ya Siha mkoa wa Kilimanjaro imefanikiwa kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa vikundi 22 vya wanawake Wilayani Siha katika mwaka wa fedha 2016/2017.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Siha Valerian Juwal alieleza hayo katika mkutano wa kawaida wa Baraza la Madiwani uliofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Siha.

Taarifa ya Mkurugenzi mtendaji ilieleza kuwa,katika mwaka wa fedha 2016/2017 halmashauri ya Wilaya ya Siha imetoa mikopo kwa vikundi  22 vya wanawake Wilayani Siha yenye thamani ya shilingi 56 ,000,000/= zikiwa ni fedha kutoka mchango wa Halmashauri wa asilimia tano (5%) ya mapato yake ya  ndani.

Aidha, Mkurugenzi katika taarifa yake alieleza Baraza kuwa pamoja na changamoto ya halmashauri kukabiliwa na vyanzo vichache vya ukusanyaji wa mapato lakini Halmashauri imejitahidi kutoa kiasi hicho cha fedha kwa vikundi vilivyoomba mikopo na vilivyotimiza vigezo vya kupata mikopo hiyo kwa kuzingatia sheria na taratibu mbalimbali.

Ametoa wito kwa vikundi vya wanawake katika wilaya ya Siha kutumia fursa hiyo ya Serikali  ya kuomba mikopo yenye masharti nafuu  katika kujikwamua kiuchumi katika ngazi ya Familia na jamii kwa ujumla wake.

Hata hivyo,Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Siha ametoa wito kwa vikundi  mbalimbali vilivyopatiwa mikopo kutumia mikopo hiyo kwa shughuli waliojipangia  badala ya kutumia mikopo waliyopewa  katika mambo yasiyoleta tija.
Alieleza kuwa pamoja na jitihada za halmashauri kutoa mikopo hiyo kwa wanawake  lakini wahusika bado wanayo wajibu mkubwa wa kuhakikisha kuwa mikopo hiyo inarejeshwa kwa wakati ili iweze kuwasaidia wanufaika wengine katika halmashauri ya Wilaya ya Siha.

Halmashauri ya Wilaya ya Siha katika upangaji wa mipango na bajeti kila mwaka inatenga asilimia 5 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya kuwawezesha wanawake na asilimia 5 ya mapato ya ndani ya Halmashauri  mikopo kwa vikundi vya vijana.


Katika mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri ilitenga bajeti ya Tsh 87,051,850 kwa ajili ya kuwezesha vikundi vya wanawake. Ambapo hadi kufikia Juni 2017 jumla ya vikundi ishirini na mbili (22) vya wanawake vilipatiwa mkopo wenye thamani ya Tshs 56,000,000/= zikiwa ni fedha kutoka mchango wa Halmashauri wa asilimia tano (5%) ya mapato ya ndani.

No comments:

Post a Comment